Pages

Friday, May 17, 2019

ALAMA YA PENZI LA KWELI

Mapenzi ni kitu kizuri kwani muanzilishi ni MUNGU  na siku zote  MUNGU NI MWEMA. Kuwa na mtu anaekupenda ni haki yako toka wa MUNGU ALIEKUUMBA na ukiona mtu hakupendi maana yake anapingana na mpango wa MUNGU katika maisha yako na ni wajibu wako kusimamia haki yako ya kupendwa kikamilifu.Ni kweli kabisa kuwa unastahili kupendwa kikamilifu ili uweze kufurahia maisha yako ya kila siku. Toka tukiwa watoto wachanga tunapokea upendo toka kwa wazazi wetu bila kutoa penzi lolote kwa wazazi wetu lakini kwa kadri tunavyokua wazazi wetu wanatarajia kuwa tutaweza kushirikiana nao na sisi kuweza kuchangia katika furaha ya maisha yao. Alama ya kwanza tuionayo kwa wazazi ni kuhangaikia mahitaji yetu yote jambo ambalo linatupatia afya na furaha ya kuwemo duniani. Kipindi hichi cha utoto tunakuwa tunategemea wazazi wetu kwa asilimia 100, yaani hata unapojisaidia mama hata angalia harufu mbaya bali kwa moyo mweupe ataondoa hali hiyo mbaya. Ili uweze kuwa na penzi la kweli na uhusiano uliojaa furaha kwa sehemu lazima utajikuta unamtegemea mpenzi wakoili ufurahia maisha yako.  Watu wengi wanashindwa  Kutengeneza mazingira ambapo penzi tamu linakuwepo kwani pale unapomtegemea mpenzi wako kukujali kwa sehemu kubwa na yeye akashindwa kukujali unajikuta unaumia japo huwezi kulia kama mtoto mchanga. UNAPORUHUSU maumivu kuendelea kuongezeka ukubwa moyoni mwako unahatarisha maisha yako mwenyewe bila kujua.ALAMA zifuatazo zitakusaidia kuelewa penzi la kweli.
1.   KUHESHIMU UHURU WA KUPENDA

Mapenzi ya kweli hayalazimishwi kwani ni kama vile mzazi halazimishwi kumlisha mtoto wake mwenyewe. Mpenzi mwenye mapenzi ya kweli atajituma bila kungojea kuombwa au kukumbushwa. Nimekutana na kesi nyingi ambazo mtu alieachwa na mpenzi wake anataka msaada toka kwangu na ninapomuuliza mara ya mwisho kumpa zawadi mpenzi wako ni lini, wengi wanasema juu ya misaada waliyoitoa, “Simu yake iliharibika aliomba Tsh.15,000/= nilimpatia” nawaambia hiyo sio zawadi huo ni msaada. Zawadi hutokea moyoni na sio machoni au masikioni, ukiona nguo ya mpenzi wako imechakaa ukamnunulia huo ni msaada. Mpenzi wako akikuomba pesa aende kutengeneza nywele saloon huo ni msaada sio zawadi. Zawadi unafikiria moyoni kuwa nikimpatia mpenzi wangu zawadi ya saa au viatu atafurahi, unanunua na kumpa surprise. Kwa hiyo basi, mtu mwenye mapenzi ya kweli atajituma yeye mwenyewe kufanya au kusema mambo yatakayochangia furaha ya mpenzi wake. Kama vili alivyojituma na kukuomba uwe mpenzi wake anapashwa ajitume katika kufanya mambo yanayokuletea raha.Watu wengi wana mapenzi toroli, toroli haliwezi kusogea bila kusukumwa kadhalika watu wenye mapenzi tolroli mpaka waambiwe ndipo wanafanya jambo tamu, haipendezi iwapo unampenda mpenzi wako.


2.   JUHUDI YA KUWA MKWELI

Mtu mwenye mapenzi ya kweli nafsi yake inafurahia ukweli na hata Biblia inaonyesha hilo, “Upendo haufurahii udhalimu bali hufurahia pamoja na kweli” (1.WAKORINTHO 13:6). Mpenzi mwenye mapenzi ya kweli atapenda kuwa muwazi kwako na yeye atataka uwe muwazi kwake. Mpenzi mwenye mapenzi ya kweli atasisitiza ukweli na hataogopa ukweli japo mara nyingine ukweli unaumiza. Katika kusisitiza ukweli na uwazi ni sehemu muhimu, ukimboa atakuambia, ukishindwa kumridhisha au kumfurahisha katika ngoma ya wakubwa au katika maongezi yenu atakuambia akitegemea utafanya juhudi kuleta mabadiliko. Simu yake itakuwa kama kitabu kilicho wazi kwako na simu yako atapenda ajue yaliomo.UKWELI utaonekana katika kutimiza ahadi zake, katika nafasi anayotoa ya kukuthibitishia kuwa anakupenda na katika kuonyesha hisia zake na mitazamo yake.

3.   UNYENYEKEVU WA KWELI

Mpenzi wa kweli anajua mwanadamu yoyote hukosea na ni mwepesi katika kukubali na kukiri makosa yake bila kujitetea tetea na kujiinua. Biblia inasema “Vivyo hivyo vijana watiini wazee; Naam, ninyi nyote jifunzeni unyenyekevu mpate kuhudumiana, kwa sababu Mungu huwapinga wenye kiburi lakini huwapa Neema wanyenyekevu”         (1 PETRO 5:5). Mpenzi wa kweli amelenga kumfurahisha mpenzi wake na hivyo anapomuumiza au kumkosesha raha mpenzi wake, nafsi yake inajisikia vibaya na hivyo anakuwa mwepesi kuomba msamaha. Na sio hilo tu bali pia ataonyesha nia na bidii ya kutokurudia kosa lolote linalomuumiza mpenzi wake.UTAONA aanatafuta njia mbalimbali za kuweza kukufurahisha bila kujali hisia zake kama BWANA YESU alivyofundisha kwa kusema  “Atakae kuwa mkubwa miongoni mwenu awe mtumishi wa wote” angalia ukosefu wa unyenyekevu toka kwa mwanamke kama baba mmoja alivonielezea kwa SMS ‘DR LOVE, MIMI NIKO NDANI YA NDOA MWAKA WA 4 mke wangu amekuwa mzigo kwangu maana analoliwaze yeye ndo anataka lifanyike na mara nyingi ameleta hasara katika miradi yetu. NIFANYEJE ABADILIKE?’’ .UNYENYEKEVU NI KIGEZO MUHIMU SANA KATIKA KUJENGA PENZI LA KWELI.

4.   ANATHAMINI NGUVU YA UWEPO WAKE

Bila shaka umeshawahi kuona mtoto wa miaka miwili au mitatu akimlilia mama yake pale anapoondoka kwenda kazini au anapotoka kwenda mbali na nyumbani. Ni dhahiri hata wewe katika historia ya utoto wako ulilia pale mama alipoondoka nyumbani jambo ambalo linashuhudia umuhimu wa uwepo wa mtu umpendae. Mpenzi wa kweli atajitahidi apate muda wa kukaa na wewe na kuwa na wewe kikamilifu. Nakumbuka secretary wangu kuniambia “Doctor na wewe unamzoeza vibaya mke wako, yaani anajua muda wako wa kurudi nyumbani na sijakuona hata maramoja unachelewa au ukitoka hapa kwenda sehemu nyingine” nikamwambia kuwa nampenda mke wangu na hivyo kumuona na kuongea nae ni sherehe kwangu. Mara nyingine baada ya kula napatwa na usingizi lakini kwa kuwa najua umuhimu wa kukaa na mke wangu sebuleni nitatafuta kitu cha kuchekesha na tukianza kucheka usingizi unapotea na tunaweza kuongea hadi saa 6 usiku. Ni muhimu sana kwa wapendanao kupata nafasi ya kukaa pamoja na kucheka pamoja kwani inaimarisha hisia za kimapenzi kwa umpendae. Ukiona mpenzi wako hathamini muda wa wewe na yeye kukaa pamoja tambua una mpenzi feki.Mpenzi wa kweli atahakikisha kuwa kuwepo kwake na wewe ni sehemu ya burudani  katika uhusiano wenu.

5.   HAOGOPI

Alama muhimu na ya ajabu ya mpenzi wa kweli ni kwamba haogopi kukuambia ukweli wote na haogopi kukosana na marafiki zake na hata ndugu zake kwa ajili yako wewe. Mfano mzuri tunaupata toka kwa Bwana Yesu, “Wakwamwendea mama yake na ndugu zake; wasiweze kumkaribia kwa sababu ya mkutano. Aakaletewa habari akaambiwa; mama yako na ndugu zako wamesimama nje wakitaka kuonana na wewe. Yesu akajibu akasema, Mama yangu na ndugu zangu ndio hawa wananosikiliza neno la Mungu na kulitenda” (LUKA 8:19-21). Kwa mfano huo tunaona ni jinsi gani mtu anavyothamini uhusiano wake na mtu ampendae kiasi haogopi wazazi wake na ndugu zake watasemaje au kujisikiaje. Iwapo unataka penzi la kweli usifanye maamuzi au uchaguzi unaoongozwa na hofu ya mtu au watu. Usiogope kumhoji mpenzi wako kwani kwa kumhoji ndio utaweza kupima penzi lake kwako, je atakusikiliza na kufanya mabadiliko au atakuwa mkatili asiejali hisia zako? Usimuone mpenzi wako kama jambazi linalo  kulazimisha ufanye mambo yanayotia nafsi yako hasara. Jambazi halijali hisia zako pale linapopora mali zako zenye gharama kubwa na kukuachia hasara kubwa sana na mara nyingine hata kukujeruhi vibaya. Mpenzi asiejali hisia zako hana tofauti na jambazi, hakikisha una mpenzi alie rafiki kwako na sio jambazi. Mpenzi wa kweli lazima atakupa kipaumbele bila kujali watu au hata nafsi yake mwenyewe.


6.   ANAJITAHIDI KUKUELEWA

Chanzo kikubwa katika mahusiano ya kimahaba kuingia katika hali ya migogoro ni mmoja kudhania ya kwamba mpenzi wake ataridhika na penzi analotoa bila kutafuta njia ya kupata uhakika wa mtazamo huo.
Haijalishi mpenzi wako anakupenda kiasi gani mtazamo wako hauwezi kuwa mtazamo wake katika kila jambo. Lazima utambue nyinyi ni watu wawili tofauti na wenye historia tofauti japo yapo mambo machache ambayo mtakuwa sawa katika mitazamo. Mpenzi mwenye mapenzi ya kweli atatafuta kuelewa mtazamo wako kwanza kabla hajataka uelewe mtazamo wake kwanza, atauliza maswali ili apate kuelewa mtazamo wako bila kukuhukumu. Pale ambapo atapata shida ya kukuelewa ataoyesha kwanini anapata shida kukuelewa na kukupa kazi ya kufafanua mambo vizuri. Mpenzi wa kweli hatakuwa mwepesi kusema “Achana na hayo” bali atapenda umueleweshe kabla hajafanya uamuzi wa kukubaliana na wewe. Huko sio ubishi bali ni kiu ya kupenda kuelewa ili awe na amani na wewe.   Katika mazingira kama hayo kila mmoja anajitahidi afahamu mahitaji ya mwingine na kufanya kazi ya kuendelea kumdhibitishia mpenzi wake kuwa bado ni wa muhimu sana. Katika mazingira ya uwazi na ukweli kila mmoja anajisikia kuwa anasikilizwa na kueleweka na hisia zake kuheshimiwa. Uonapo mpenzi wako hakusikilizi au anadharau hisia zako lazima uhusiano wenu utadhurika, je utajuaje kama mpenzi wako anakupenda iwapo hataki kukusikiliza? Utajuaje kama mpenzi wako anakupenda iwapo hajali hisia zako? Utajuaje kama mpenzi wako anakupenda kama hakuhurumii? Utajuaje kama mpenzi wako anakupenda iwapo hakujali? Utajuaje kama mpenzi wako anakupenda iwapo hakusaidii unapokuwa na shida, hakulindi dhidi ya vicheche wanaokunyemelea au ndugu wanaowachonganisha, hakujali unapokuwa na huzuni, hakutii moyo unapokuwa umekata tamaa, haombi radhi anapokuwa amekosea au hakubembelezi au kukupa zawadi za hapa na pale,.JE anapokuambia anakupenda anamaanisha nini? Ni kweli kila mmoja ana mapungufu yake lakini ni  muhimu usisitize penzi la kweli na llenye furaha  .

   
 


7.   TENDO LA NDOA LINAPEWA KIPAUMBELE

Tendo la ndoa ni la kipekee kabisa katika uhusiano wa kimahaba, eneo ambalo marafiki na ndugu hawaruhusiwi kabisa kufika au kusogelea. Kutokana na upekee wake huo tendo la ndoa ni kiungo cha kipekee na muhimu kwa uhai wa uhusiano wa kimapenzi. Tafiti zinaoyesha iwapo tendo la ndoa (Ngoma ya wakubwa) linaenda vizuri litachangia furaha na ubora wa uhusiano kwa asilimia kati ya 15 – 20, lakini tendo hilo lisipokuwa na utamu toshelevu litachangia asilimia 80 – 85 ya migogoro inayojitokeza miongoni mwa wapendanao. Tendo la ndoa linapunguza makali ya vichocheo(Hormones) vinavyosababisha hasira. Pale mtu anapofika kileleni kichocheo cha OXYTOCIN humiminwa kwa wingi na kufanya mtu ajisikie amani katika mwili na nafsi yake. OXYTOCIN pia huondoa hofu na mtu anaanza kumzoea mtu kwa urahisi baada ya kushiriki nae tendo la ndoa. Hivyo basi upo umuhimu mkubwa kwa mpenzi wa kweli kukuonyesha kuwa anatoa kipaumbele kwa tendo la ndoa.

No comments:
Write comments

Recommended Posts × +